PRINCE MEDIA TZ PRINCE MEDIA TZ Author
Title: Rais Magufuli atimua muwekezaji Shinyanga
Author: PRINCE MEDIA TZ
Rating 5 of 5 Des:
Rais wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ameagiza muwekezaji wa kiwanda cha nyama cha Triple S mjini Shinyanga aondolewe...
Rais wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ameagiza muwekezaji wa kiwanda cha nyama cha Triple S mjini Shinyanga aondolewe haraka, na atafutwe muwekezaji mwingine anayeweza kufanya kazi hiyo kwa wakati.
Rais Magufuli akiwahutubia wakazi wa Shinyanga katika kilele cha maadhimisho ya sherehe za miaka 53 ya Mapinduzi ya Zanzibar zilizofanyika katika uwanja wa Kambarage mkoani humo

Rais Magufuli amefikia hatua hiyo kutokana na muwekezaji huyo kuchelewa kuanza shughuli za usindikaji wa nyama licha ya kupewa kibali kwa kipindi kirefu cha zaidi ya miaka 10, huku wafugaji wakiwa hawana mahala pa kuuza mifugo yao.
Ametangaza uamuzi huo leo katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga, ambao licha ya kuwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi mkoani Shinyanga, pia ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 53 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ambayo kwa mwaka huu sherehe zake zimefanyika katika pande zote mbili za muungano.
Amesema muwekezaji huyo amepewa kibali cha kujenga na kuendesha kiwanda cha nyama kwa kipindi kirefu tangu yeye akiwa Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, hadi akahamishiwa Wizara ya Ujenzi na sasa ni Rais, lakini hakuna kilichofanyika.
Kutokana na hali hiyo ameutaka uongozi wa mkoa huo, Wizara ya Viwanda pamoja na Wizara ya Kilimo,Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi kufuta mradi wa kiwanda cha kusindika minofu ya nyama cha Triple S kutokana na mwekezaji huyo kukaa muda mrefu bila kiwanda hicho kufanyakazi.
Rais Magufuli akipunga mkono kuwasalimia wananchi wa Shinyanga waliofika katika uwanja wa mpira wa Kambarage katika kilele cha Maadhimisho ya Sherehe za miaka 53 ya Mapinduzi ya Zanzibar mkoani humo Januari 12,2017
"Viongozi wa mkoa, idara, taasisi husika za serikali na wizara futeni huu mradi wa kiwanda cha nyama cha Triple S, haiwezekeni tusubiri mtu miaka 10 huku wafugaji wanahangaika na mifugo yao, ndiyo maana wengine wanahamahama, sasa wakihama mnawaambia wauze ng'ombe, sasa watauza wapi kama kiwanda hakuna. Kuna wakati tulitaka kumfuta huyu muwekezaji wa Triple S, wanasiasa wakamtetea, nadhani sasa hawatamtetea tena". Amesema Rais Magufuli.
Mbali na agizo hilo, amewataka watendaji katika mamlaka husika za serikali kutowakwamisha viongozi hao kuweka muwekezaji mwingine, na kusema "Kama kuna mtu atawakwamisha, niambieni mimi nitamkwamua"
Rais Magufuli pia ameuagiza uongozi wa mkoa wa Shinyanga kufuta leseni ya Mwekezaji aliyetaka kuchukua machimbo ya wafanyabiashara wadogowadogo zaidi ya 15,000 katika eneo la Mwakitoliyo Wilaya ya Shinyanga vijijini.
Hayo ni maamuzi ya pili katika ziara hiyo dhidi ya wawekezaji, ambapo jana akiwa mkoani Simiyu alimzuia muwekezaji wa uchimbaji wa madini ya Nikel kuendelea na uchimbaji ili eneo hilo pawekwe tanki ya maji kama ilivyokuwa imepangwa awali, na kusema kuwa muwekezaji huyo siyo muhimu zaidi ya wananchi maelfu wanaoteseka kwa kukosa huduma ya maji. 
Rais Magufuli akielekea kuwahutubia wakazi wa Shinyanga katika kilele cha Maadhimisho ya sherehe za miaka 53 ya mapinduzi ya Zanzibar zilizofanyika katika uwanja wa Kambarage mkoani humo

About Author

Advertisement

Post a Comment

 
Top