PRINCE MEDIA TZ PRINCE MEDIA TZ Author
Title: WAMILIKI WA MADINI WATAKIWA KUIIGA TANZANITEONE
Author: PRINCE MEDIA TZ
Rating 5 of 5 Des:
    Mkuu wa Mkoa wa Manyara Alexander Mnyeti akizungumza na wadau wa madini mjini mirerani      Mwandishi Wetu,Arusha Mirerani. M...
 
 Mkuu wa Mkoa wa Manyara Alexander Mnyeti akizungumza na wadau wa madini mjini mirerani 
 
 
Mwandishi Wetu,Arusha

Mirerani. Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Alexander Mnyeti amewataka wamiliki wa migodi ya madini ya Tanzanite kuiga kampuni ya TanzaniteOne kwa kusaidia miradi ya jamii na kuachana na mtindo wa kuchuma na kuondoka bila kuchangia chochote. 

Mnyeti aliyasema hayo jana wakati akizindua madarasa matano ya shule ya msingi Songambele Mji mdogo wa Mirerani, Wilayani Simanjiro, yaliyojengwa na kampuni ya TanzaniteOne. 

Alisema wamiliki wengi wa madini ya Tanzanite huwa wanachimba na wakipata wanakwenda kuwekeza kwenye mikoa ya jirani ya Arusha na Kilimanjaro. 

"Wamiliki wa migodi mnapaswa kubadilika igeni mfano wa kampuni ya TanzaniteOne ambayo inasaidia jamii kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo," alisema Mnyeti. 

Alisema jamii ya eneo hilo ingefurahi kuona faida ya uwepo wa madini hayo kwa wamiliki hao kurudisha kidogo walichokipata kwa kuchangia maendeleo. 

Mwalimu mkuu wa shule hiyo, Mwanahamisi Musa alisema TanzaniteOne imejenga madarasa hayo baada ya kubaini baadhi ya wanafunzi wanasoma nje sababu ya mafuriko yaliyotokea Machi mwaka 2013 na kuharibu vyumba saba. 

Mwalimu Musa alisema mafuriko hayo pia yaliharibu ofisi ya walimu, choo cha wanafunzi na nyumba mbili za walimu. 

"Vyumba saba vya madarasa vilizuiwa na mhandisi wa wilaya hiyo visitumike kutokana na nyufa zilizohatarisha usalama wa wanafunzi," alisema mwalimu Musa. 

Alisema kutokana na uharibifu wa mafuriko hayo, shule hiyo ilibakiwa na vyumba vitano pekee ambavyo walivitumia kufundishia wanafunzi 1,158. 

Alisema shule hiyo iliyoanzishwa mwaka 2002 ina wanafunzi 1,158 wavulana 602 na wasichana 556 hivyo madarasa hayo yatapunguza msongamano. 

Alisema wanaishukuru kampuni ya TanzaniteOne kwa kukamilisha madarasa hayo ila wanawaomba wamalizie vyumba viwili vya madarasa, ofisi ya walimu na kisima cha maji kama walivyoahidi. 

Ofisa mahusiano wa kampuni ya TanzaniteOne, Halfan Hayesh alisema atafikisha salamu za pongezi zilizotolewa na mkuu huyo wa mkoa kwa viongozi wake. 

Hayeshi alisema pia atafikisha ombi la kutakiwa wamalizie vyumba viwili vya madarasa, ofisi ya walimu na kisima cha maji kama walivyoahidi.

About Author

Advertisement

Post a Comment

 
Top