PRINCE MEDIA TZ PRINCE MEDIA TZ Author
Title: RIPOTI YA TAKUKURU YAZIDI KUCHAFUA HALI YA HEWA BUNGENI
Author: PRINCE MEDIA TZ
Rating 5 of 5 Des:
Naibu Spika,Job Ndugai akiwaonya waabunge wa  Upinzani bun geni jana kabla ya kutokea mtafaruku. Picha na fidelis Felix  Dodoma. Sakata ...



Naibu Spika,Job Ndugai akiwaonya waabunge wa  Upinzani bun geni jana kabla ya kutokea mtafaruku. Picha na fidelis Felix 

Dodoma. Sakata la uchotaji wa Dola za Marekani 200 milioni katika akaunti ya Tegeta Escrow limeendelea kuibuka kwa sura mbalimbali bungeni. Safari hii, Bunge limetakiwa kueleza ni kwa nini Ripoti ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) isifikishwe katika chombo hicho cha kutunga sheria sambamba na ile ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).


Hayo yalijitokeza bungeni jana baada ya wabunge kadhaa kusimamia wakitaka mwongozo wa Spika kuhusu uchunguzi huo, hasa kutokana na kuwapo taarifa kuwa ripoti ya CAG itawasilishwa bungeni mwishoni mwa mwezi huu, lakini ile ya Takukuru ambayo pia inachunguza suala hilo, haitapelekwa bungeni wala kujadiliwa.


Uchunguzi wa Akaunti ya Escrow uliamuliwa na Serikali baada ya Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila kulipua ufisadi uliotokana na utata katika uchotaji wa fedha kwenye akaunti hiyo katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT) baada ya kutokea mgogoro wa kibiashara baina ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na Kampuni ya kufua umeme ya IPTL.


Katika mgogoro huo, Tanesco ilikuwa inabishia kiwango cha fedha ilichokuwa inalipa kwa gharama za uwekezaji kwa IPTL, ndipo ikaamuliwa na Mahakama ifunguliwe akaunti hiyo ili fedha ilizokuwa inalipa ziendelee kuwekwa huko hadi mgogoro utakapokwisha. Kesi hiyo iliamuliwa katika mazingira yanayoelezwa kuwa na utata na fedha hizo kuchukuliwa haraka na IPTL.


Jana, baada ya kipindi cha maswali na majibu, wabunge kadhaa walisimama wengi wakiwa wa upinzani wakitaka mwongozo kuhusu lini ripoti hizo mbili zitawasilishwa bungeni hasa baada ya ile ya Takukuru kuelezwa na Mkurugenzi Mkuu wake, Dk Edward Hoseah kuwa imekamilika na kukabidhiwa kwa Waziri Mkuu.


Mbunge wa Arumeru Mashariki (Chadema), Joshua Nassari ndiye aliyefungua mlango wa kuomba mwongozo wa Spika akitaka kujua ni lini ripoti hiyo itawasilishwa na kwa nini isiambatane na ile ya CAG kwa kuwa zote zinatokana na maazimio ya Bunge kutaka uchunguzi huo ufanyike.


Pia Nassari alihoji kwa nini mjadala wa ripoti ya CAG umepangwa siku mbili za mwisho kabla ya kumalizika kwa mkutano wa Bunge.


“Naomba maelezo kwa nini hii ya Takukuru haitaletwa wakati imeelezwa kuwa Waziri Mkuu ameshakabidhiwa?” alihoji Nassari.


Akijibu, Naibu Spika, Job Ndugai alisema Kamati ya Uongozi imeshajadili suala hilo na kuamua kwamba ripoti ya CAG itapitia kwenye Kamati ya PAC inayoongozwa na Zitto Kabwe na kuwasilishwa bungeni.


“Ripoti ya CAG itawasilishwa kwenye Kamati ya PAC na wabunge mtakabidhiwa nakala kama tulivyokubaliana kwenye Kamati ya Uongozi,” alisema Ndugai na kuongeza:


“Ripoti itawasilishwa tarehe 26 mwezi huu kama ilivyorekebishwa kwenye ratiba. Kuhusu suala la kupangwa mwishoni ni suala la kanuni kwa kuwa huwa tunaanza na shughuli za Serikali kwanza halafu ripoti zinafuata.”


Kuhusu ripoti ya Takukuru, Ndugai alisema haiwezi kuwasilishwa bungeni kwa kuwa taasisi hiyo ikishamaliza shughuli zake inaweza kuchukua hatua kwa kupeleka taarifa kwa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kwa ajili ya hatua zaidi.

About Author

Advertisement

Post a Comment

 
Top