PRINCE MEDIA TZ PRINCE MEDIA TZ Author
Title: NJAA INAVYOSABABISHA UTORO KWA WANAFUNZI WA SHULE ZA MSINGI LONGIDO
Author: PRINCE MEDIA TZ
Rating 5 of 5 Des:
    Baadhi ya wananfunzi wa Shule ya Msing Orbomba wakiwa wanajisomea majarida mbalimbali    NA: Andrea Ngobole, Longido Kati ya watot...

 

 



Baadhi ya wananfunzi wa Shule ya Msing Orbomba wakiwa wanajisomea majarida mbalimbali 

 

NA: Andrea Ngobole, Longido

Kati ya watoto kumi wa shule ya Msingi Orbomba wilayani Longido Mkoani Arusha ni watoto sita tu ambao hufika shule na kuhudhuria masomo, hii ni Zaidi ya asilimia arobaini ya watoto wote wanaotakiwa kufika shule. Njaa imesababisha wanafunzi washindwe kuhudhuria masomo. 


Hali iliyopo katika shule hii ndiyo picha halisi iliyopo katika shule za msingi 43 zilizopo wilayani Longido. Vijiji vingi vya wilaya ya Longido vinakabiliwa na ukame na hatimaye kuleta njaa kali katika familia kiasi kwamba watoto wanashindwa kwenda shule.

 

Upatikanaji wa lishe bora na salama kwa matumizi ya wanadamu ni moja ya huduma ya lazima kwa maisha na ustawi wa wanadamu. Kwa mujibu wa Sera ya Lishe Bora ya mwaka 1992 inasema lishe ni mchakato wa chakula mwilini na ni vyema kila mwanadamu kuzingatia makundi matano ya chakula yanayomsaidia kuwa na afya bora ambayo ni nafaka, matunda, mbogamboga, nyama na mafuta ili kuepukana na madhara ya utapiamlo.

Katika wilaya ya Longido wanavijiji wengi hawana uwezo wa kupata mlo kamili kutokana na hali ngumu ya maisha waliyonayo iliyosababishwa na athari za mabadiliko ya tabianchi.

 

Familia nyingi za vijiji vya, Kimokowa, Ranchi, Kitumbeine, Ortepesi, Orbomba, Ranchi, Orpukeli, Kitumbeine, Ildonyo, Noondoto na Gilailumbwa

hazimudu kununua chakula cha kulisha familia zao kutokana na mifugo yao kufa kwasababu ya ukame uliyoikumba wilaya hiyo misimu minne mfululizo kuanzia mwaka 2020-2023 

Norikidoti Kimamwe (42) mkazi wa kijiji cha Kitumbeine anasema Ukame umepelekea kukosa mifugo na hawapati chakula kwa ajili ya familia.

 

“Yaani kwa siku tunakula mlo mmoja tu kwani bei ya chakula ni ghali sana hatuwezi kumudu gharama zake debe la mahindi sokoni ni shilingi 24000 sasa kiasi hicho ni kikubwa sana kwangu na familia yangu”. alisema


Jacob Kipamba (27) mkazi wa kijiji cha Ranchi anasema ukosefu wa chakula ni mkubwa sana kijijini hapo kwa sababu wanategemea mifugo wauze ndiyo wanunue chakula, ukame umepelekea ng’ombe kufa, alikuwa na ng’ombe 16 ambapo walikufa 8 amebakiwa na ngombe 8 na mbuzi wanne.

“Mimi kwa kuwa nafanya kazi ya ulinzi katika ofisi ya kijiji kidogo napata mshahahara unaowezesha kununulia familia chakula, ila kama unavyojua ukubwa wa familia ukipata chakula mtoto wa kaka au dada huwezi kumuona ana njaa ukaacha kumsaidia,” alisema

 

Familia hizi ni sehemu ya jamii kubwa ya wananchi wa wilaya ya Longido waliokumbwa na baa la njaa baada ya mifugo yao kufa kwa ukame uliosababishwa na mabadiliko ya tabianchi hali iliyosababisha mahudhurio hafifu na utoro kwa wanafunzi wa shule za msingi. 

Wazazi hawa wanadai watoto wao wanashindwa kwenda shuke kwa sababu wanakosa hata uji wa kuwapikia asubuhi na kwenda shule bila kutia kitu chochote tumboni na hivyo njaa inawapelekea kusikia kizunguzungu na kushindwa kuhudhuria shule kwa ajili ya masomo.

Pamoja na serikali kupeleka mahindi ya bei nafuu katika wilaya hii wakazi hao wanashindwa kununua mahindi hayo yanayouzwa shilingi elfu themanini kwa gunia moja la kilo mia moja kwani masharti ya serikali ni kuuza kwa gunia na siyo kwa debe moja.

 

Bei ya mahindi Katika soko la Longido yanauzwa na wafanyabiashara wa kawaida kwa shilingi 135,000 kwa gunia na bei ya debe moja la mahindi linauzwa kati ya shilingi 24000/= mpaka 30,000/= ambapo kama serikali ingeuza mahindi yake kwa debe moja wangeuza kwa shilingi 16,000/=

 

Mwalimu wa Shule ya Msingi Orbomba ambaye hakutaka kutajwa jina lake kwa kuwa siyo msemaji wa shule na mkuu hakuwepo anasema kijijini hapo kuna njaa sana hali ambayo inaathiri utendaji kazi wao darasani kwani wanafunzi wamekuwa watoro hawaji shule kwa sababu ya njaa na pia hata wanaokuja ikifika mchana wanatoroka kwani wanashindwa kuvumilia njaa.

“Kimsingi mahudhurio ya watoto shuleni hapa ni madogo kutokana na njaa, walimu pia tunashindwa kuendelea na vipindi vya mchana kwani usikivu na uelewa wa watoto unakuwa mdogo sana kwa sababu ya njaa,” anasema 

Anasema wameongea na wazazi wawe wanachanga shilingi 18,000 kwa muhula ili waanze utaratibu wa kuwapikia chakula hapo shuleni ila bado mwitikio siyo wa kuridhisha kwani nao wanasema hawana pesa. 

Shule hiyo yenye jumla ya wanafunzi 445 ambapo mahudhurio ni wastani wa asilimia 60 na asilimia 40 hawahudhurii shule kabisa kutokana na njaa.

Aidha baadhi ya watoto hao hulazimika kwenda mjini kuomba chakula kwa wasamaria wema ili waweze kupeleka nyumbani kwa ajili ya mlo wa familia.

Afisa Elimu msingi wilaya ya Longido, Deusdedit Bimbalirwa amekiri kumekuwepo na utoro katika shule za msingi kutokana na tatizo la njaa.

Bimbalirwa alisema kuna baadhi ya wanafunzi wameondoka na wazazi wao kwenda kutafuta malisho ya mifugo.

"Kawaida hizi jamii ukame unapokuwa mkali huwa wanahama na mifugo sasa na wanafunzi wanahama nao" alisema

Alisema pia kutokana na njaa wanafunzi wanapungua madarasani na kurudi majumbani.

Hata hivyo, alisema tayari Halmashauri ya Longido imeanza kulifanyiakazi tatizo hilo kwa kupeleka mashuleni na vijijini chakula cha msaada na bei nafuu. 

"Tayari chakula cha msaada kimeanza kupelekwa mashuleni lakini pia chakula cha bei nafuu ili kukabiliana na hali hii" alisema 

Kutokana na uhaba wa chakula unaokabili familia nyingi wilayani hapa, baadhi ya mashirika kadhaa yasiyo ya kiserikali yanayotekeleza miradi katika wilaya hii ya Longido yameanza kusambaza chakula cha bure kwa kaya zilizokumbwa na njaa.

Kaimu Afisa Kilimo wa wilaya ya Longido, Mariam Fivawo anasema ukame umesabisha uhaba wa chakula katika maeneo mengi ya wilaya hiyo ambayo asilimia 95 ya wananchi wake ni wafugaji.

 

 

 

About Author

Advertisement

Post a Comment

 
Top